Mchungaji: Wakili wa Umisheni
Pastor Azaki Nash
Kusudi la Mungu la ukombozi lililotimizwa katika Kristo Yesu na kuenezwa na mitume linabaki kuwa kazi ya Kanisa hadi Kristo atakaporudi. Wakati kanisa linapoelewa hili, kila kitu kinabadilika. Hapa ndipo penye jukumu la wachungaji kuhakikisha kwamba makanisa yao yamejikita katika umisheni.
Jukumu letu kama wachungaji hutupatia ushawishi wa kipekee katika kuelekeza kipaumbele cha kusanyiko kuelekea umisheni. Hii inatuhitaji kuwa na ari na mkakati wazi wa kutangaza umisheni wa ndani na nje ya nchi. Kusanyiko linapomwona mchungaji amekamatwa na mawazo haya, litafurika katika ushiriki wao katika kuwa kanisa linalofadhili umisheni na kutuma wamishenari.
Katika mwaka wa 2020, wakati wa janga la COVID, kanisa langu lilikuwa likifadhili wamishenari wa ndani 100 na wake zao wanaohudumu na Jumuiya ya Wamishenari ya Kiinjili (EMS) ya ECWA. Zaidi ya hayo, tulitoa msaada wa mara moja kwa mashirika na makanisa mengine ya kimishenari. Hili liliwezekana kwa sababu mchungaji ambaye alitangulia kabla yangu alikuwa na moyo wa umisheni.
Baada ya kushika nafasi kama mchungaji kiongozi mpya, niliazimia kuendeleza urithi huu kwa kuongezaahadi yetu ya umisheni. Haikuwa vigumu kupata ushirikiano wa kusanyiko ili kuongeza kutok a wamishenari 100 hadi 125 mwaka wa 2021.
Jambo la msingi ni kwamba kanisa langu, ECWA Wuse II Abuja, Nigeria, liko kwenye umisheni kwa sababu wachungaji waliofuata waliweka msisitizo wa lazima kwenye umisheni. Mchungaji anapofikiri na kuzungumza umisheni, kusanyiko hujifunza kushiriki kikamilifu katika utume wa Mungu. Kila kanisa linapaswa kuwa na njia hii.
Mchungaji anapofikiri na kuzungumza umisheni, kusanyiko hujifunza kushiriki kikamilifu katika utume wa Mungu.
Lazima nisisitize kwamba uhamasishaji kwa ajili ya umisheni wa nje ya nchi unaweza kuwa mgumu ikilinganishwa na umisheni wa ndani. Ikiwa sarafu ya taifa italinganishwa na dola na kuwa na thamani ya chini sana, kile kinachoonekana kuwa ni kiasi kikubwa kitashuka thamani inapobadilishwa na kutumika katika nchi za kigeni. Suluhisho la busara ni kuongeza kiasi cha ufadhili, tuseme kwa kuzidisha mara dufu kile anachostahili mmishenari wa ndani. Hali hii inaonyesha kwamba wachungaji wanapaswa kufahamu wenyewe hadithi halisi za umishenari, mahitaji ya maombi, na changamoto.
Kama mawakili wa rasilimali za Mungu, wachungaji pia wanawajibika kutumia rasilimali kwa busara na usikivu wa kiroho mahali ambapo Roho Mtakatifu anaongoza (Efe. 1:17 18). Ni wajibu kwa wachungaji kuwa mawakili wazuri wa umisheni na wamishenari. Tunaweza kutumia kwa makusudi huduma zetu za ibada ya Jumapili ili kutoa taarifa za mara kwa mara za umisheni.
Kila mchungaji ambaye atakuwa na ufanisi katika kuhamasisha umisheni lazima aondoe maslahi binafsi, hata wakati ambapo timu ya uongozi inasitasita kutumia zaidi kwa ajili ya mmishenari kuliko kwa mchungaji wao. Zaidi ya fedha, nyenzo na vitu, na rasilimali watu, kila shirika la kimishenari huthamini maombi ya watakatifu. Wachungaji wanapaswa kukusanya watu kuomba mara kwa mara kwa ajili ya umisheni.
Mimbari inatoa fursa ya kimkakati ya kutoa changamoto kwa washarika kuishi kimisheni kwa ajili ya Kristo. Wachungaji wanapohubiri Neno kwa uaminifu na kuwafundisha washirika kuwafikia waliopotea, kanisa litakuwa na waamini walio na nia ya utume. Huu umekuwa uzoefu wetu.
Kwa kumalizia, ninawaalika wachungaji wenzangu kujenga shauku ya umisheni, ili makanisa yetu yachochewe kwenda katika mataifa yote na Injili ya Yesu Kristo. Wito wetu kama wachungaji ni fursa ambayo tutaitolea hesabu atakapotokea Bwana wetu. Kwa hivyo, ninatoa wito kwa wachungaji wote kufanya kazi katika kujenga makusanyiko yenye afya na yenye kustawi ambayo yanapanua mipaka ya umisheni ndani na nje ya nchi—kwa ajili ya utukufu wa Kristo ambaye ametuingiza katika utume wake wa nyakati za mwisho (2 Wakor. 5:19-20).
Azaki Nash ni mhudumu wa chuo kikuu, mwandishi hodari, mchungaji, na mmisiolojia. Mafunzo yake ya kihuduma yanajumuisha Diploma ya baada ya kuhitimu ya Theolojia (PGDTh), shahada ya pili ya Divinity (MDiv), M.A. katika Uongozi na Usimamizi wa Shirika, na PhD katika Misiolojia. Yeye ni Mchungaji Kiongozi wa ECWA Wuse II Abuja, Nigeria. Ameoa na ana watoto wawili.