fbpx Skip to content

Kutafakari Tena Somo La Antiokia Je, Wachungaji Wanasikiliza?

Sura ya 13 ya kitabu cha Matendo ya Mitume inaelezea kanisa ambalo lilikuwa katika sehemu ya Shamu (kwa sasa ni nchi ya Syria) ambalo lilikuwa ni la kwanza kutuma rasmi wamishenari kwenda nchi nyingine, kwenye utamaduni mwingine katika kipindi cha kanisa la Agano Jipya.

“Na katika kanisa la huko Antiokia, palikuwa na manabii na walimu, nao ni Barnaba, na Simeoni aitwaye Nigeri, na Lukio Mkirene, na Manaeni aliyekuwa ndugu wa kunyonya wa mfalme Herode, na Sauli. Basi hawa walipokuwa wakimfanyia Bwana ibada na kufunga, Roho Mtakatifu akasema, Nitengeeni Barnaba na Sauli kwa kazi ile niliyowaitia. Ndipo wakiisha kufunga na kuomba, wakaweka mikono yao juu yao, wakawaacha waende zao”. (Matendo ya Mitume 13:1-3).

Inaonekana baadhi ya watu walioorodheshwa katika kisa hiki ni sawa na wachungaji wa leo. Walikuwa wakimtumikia Bwana kwa pamoja katika kuomba na kufunga. Ingawa hatujaambiwa dhahirini masuala gani ambayo walikuwa wakiyaombea na kufunga, lakini bila shaka mioyo yao ilikuwa pamoja na Bwana, na ndiyo maana Bwana alizungumza nao. Bwana aliwataka viongozi hawa kutoka kanisa la Antiokia kumtengea Barnaba na Paulo kwa ajili ya kazi ambayo alikuwa amewaitia. Baada ya kutengwa huko kwa Barnaba na Paulo, yaliyoendelea ni historia (hayatuhusu). Antiokia lilikuwa ni kanisa lenye wachungaji wanaosikiliza, wachungaji na viongozi waliokuwa na mguso mkubwa katika ulimwengu hata kuzidi kanisa la Yerusalemu lenyewe.

Jambo la muhimu hapa ni hili: Wakati agizo kuu lilipotolewa na Kristo kuwaamuru wafuasi wake kuwa mashahidi wake kote hadi mwisho wa dunia, hakuna mtu ambaye angetabiri kwamba kanisa lililoanzishwa huko mbali kabisa katika nchi ya Syria lingekuwa na ushawishi wa kushangaza katika ulimwengu. Kama ungeniuliza mimi juu ya kitu gani kilileta tofauti, ningesema, ni “viongozi wanaosikiliza”,

Ni kweli, wakati Petro akiwa bado huko Yerusalemu akitetea uwepo wake nyumbani mwa Kornelio, Mungu alikuwa tayari akiinua viongozi katika kanisa la Antiokia kupitia Roho wake. Viongozi hawa waliweza kusikiliza sauti yake wakati walipokuwa wanaendelea kumtumikia Mungu na kumwabudu. Walikuwa manabii na walimu, na walikuwa makini kwa Bwana. Mioyo yao ilikuwa ulipokuwepo moyo wa Bwana, na Bwana aliwakuta wakiwa tayari kubeba agizo lake. Mungu aliwapa fursa ya kumtuma mmoja wa mitume wakuu waliowahi kutokea duniani. Na matokeo ya utume huo yalikuwa ni kuandikwa kwa takribani theluthi mbili ya vitabu vya Agano Jipya. Mtume Paulo, pamoja na washirika wake, alikuwa miongoni mwa watu waliokuwa na ushawishi mkubwa katika vitabu vya Agano Jipya vilivyokubaliwa.

Hiyo iliwezekanaje? Ilikuwaje kanisa ambalo lilianzishwa na wahamiaji walioteswa na wakawa wakimbizi kupokea sehemu ya heshima na umuhimu katika mpango wa kazi ya Mungu wa ukombozi katika ulimwengu? Walikuwa na viongozi au wachungaji waliokuwa wasikivu kwa Mungu. Walifunga, walihudumu na walisikiliza.

Wachungaji ni watu muhimu sana katika jambo ambalo Mungu anaweza kulifanya kwa kanisa lake. Si ajabu Paulo aliwaonya wazee wa Efeso kwa kuwaagiza kujitunza wao wenyewe na kulitunza kundi ambalo Roho Mtakatifu aliwaweka kuwa wasimamizi. Wachungaji hawa wangeweza kulikuza au kuliangamiza kundi. Wangeweza kuwatia moyo watu wa Mungu katika wito wao mkuu au kuwazuia wasiusikie wito huo. Wanachukua nafasi ya kushangaza katika maisha ya kanisa la Mungu na watu wake. Ni Makanisa mangapi kama ya Antiokia ambayo Mungu anayo huko ulimwenguni, yenye wachungaji watakaoweza kuisikiliza sauti yake?

Wito huu bado unaendelea hata leo, na wachungaji wasikivu bado wanausikia. Sababu ambazo Mungu alitaka atengewe Barnaba na Paulo bado ni zile zile hata leo. Paulo ameziandika kwa muhtasari katika Matendo 26:18, “Uwafumbue macho yao, na kuwageuza waliache giza na kuielekea nuru, waziache na nguvu za Shetani na kumwelekea Mungu; kisha wapate msamaha wa dhambi zao, na urithi miongoni mwao waliotakaswa kwa imani iliyo kwangu mimi”.

Watu wengi bado wanaishi na kufa bila kuisikia habari njema za Mungu. Zipo jamii nyingi leo, majiji na miji ambayo bado haimjui Kristo kabisa, au sehemu ambazo Yesu aliwahi kujulikana hapo kabla lakini kwa sasa hajulikani tena. Mungu aliyeliita na kuliagiza kanisa laAntiokia bado anaita na kutuma leo: “Nitengeeni!” Je, wachungaji wanamsikia? Kama wewe ni Mchungaji, uko tayari kufanya nini kuhusiana na wito huu?

Picha: Mch. Dk. Joshua Bogunjoko, Mkurugenzi wa SIM Kimataifa.

share
share
Instagram
contact us
contact us
contact us