fbpx Skip to content

Wajibu Wa Biashara Katika Umisheni

Kehinde Ojo

Kuna hadithi moja inayohusu kundi la watu walioishi karibu na pwani. Baada ya miaka kadhaa wakishuhudia ajali za kuzama kwa meli baharini na matokeo yake ni kupotea kwa maisha ya watu na mali, waliamua kufanya jambo fulani kuhusu hali hiyo. Walijenga kibanda karibu na pwani kwa ajili ya kuwahifadhi waathirika wa ajali hizo. Mtu mmoja alitoa wazo la kuweka pia mgahawa ili kuwasaidia wale waliokuwa wanaokolewa kupata chakula na vinywaji kwa urahisi. Kwa vile ajali za meli hazitokei mara kwa mara, kulitokea wazo la kuuza vitafunwa pamoja na vinywaji kwa wateja wengine wakati hakuna ajali ya meli. Hivyo biashara ilikua vizuri. Walakini, ilipotokea ajali ya meli, hakuna mtu aliyejali kama kuna ajali ya meli imetokea! Kwa hiyo kusudi la mwanzo la kuanzisha kibanda kwa ajili ya waathirika wa ajali za meli likawa limeshindikana.

Akaita watu kumi katika watumwa wake, akawapa mafungu kumi ya fedha, akawaambia, “fanyeni biashara hata nitakapokuja” (Luka 19:13).

Katika masimulizi kutoka kitabu cha Luka, maelekezo ya Bwana mkubwa kwa watumishi wake yaliwataka watumie pesa alizowapa kufanyia biashara mpaka atakaporudi. Kwa hiyo, kitu muhimu kabisa walichotakiwa kufanya wale watumishi ni kuwekeza zile pesa katika biashara wakati wanamsubiri bwana wao. Motisha ya kufaulu katika biashara hii ilikuwa ni kumfurahisha bwana wao kwa kupata faida atakaporudi. Hivyo, maana ya biashara siyo tamaa ya watumishi kufanya watakacho, bali furaha ya bwana wao kupata faida ya pesa zake. Basi, siyo biashara kama biashara tu, bali biashara kama kazi kamilifu katika mtazamo wa bwana wao.

Ni katika ufahamu huu ndipo akili zetu sisi Wakristo zinapowekwa huru kutumia biashara au kazi mbalimbali nchini mwetu au kutoka nje ya nchi kama zana za utumishi. Kiuhalisia, maswali ambayo Wakristo wafanyabiashara wanapaswa kumuuliza Mungu, ni haya, ‘Ni nini unataka nifanye ni timize kwa ajili yako kupitia biashara hii? Na, ‘Ni kwa namna gani biashara hii inatakiwa ikutumikie pamoja na kusudi lako?’ Suala moja kubwa tunalopaswa kulitatua haraka katika shughuli zetu tofauti tofauti , na hata katika maeneo mengi ya maisha yetu, ni suala la umiliki. Ni nani ananimiliki mimi? Ni nani anamiliki biashara yangu? Ni nani anamiliki taaluma yangu? Ni nani anamiliki rasilimali zangu ambazo zimewekwa chini ya uangalizi wangu?

Katika toleo hili, utajifunza jinsi Mungu anavyofanya kazi huko Afrika Kaskazini akitumia biashara na elimu kuwaunganisha wenyeji kupitia mkakati wa “Nenda Kaskazini”. Utasoma simulizi za kushangaza kuhusu uaminifu wa Mungu katika maisha ya Mchungaji Johnson Asare, msomi, mmishonari na mfanyabiashara, na katika maisha ya Bwana Septi Bukula, kiongozi wa umisheni na mfanyabiashara. Utafahamu jinsi hadithi ya Msamaria Mwema, kama ilivyotumiwa na Mchungaji Asare ilivyosaidia ufahamu wake wa kibiashara na kazi ya umisheni. Ndugu Bukula anashirikisha ufahamu wake juu ya masomo aliyojifunza kutoka kwa baba yake kuhusu kufanya kwa pamoja biashara na umisheni, ukilinganisha na yale mahubiri yaliyokuwa yanaenezwa na makanisa yakikatisha tamaa kwa kudai kuwa Wakrsito wanatakiwa kupokea baraka lakini hawahusiki kutumia utajiri wao kwa ajili ya watu wengine.

Ni shauku yangu kuwa toleo hili litafungua macho yako kuona fursa nyingi zilizoko katika ulimwengu wa umisheni, na hasa katika eneo la biashara, na Mungu atakutumia wewe pamoja na mazingira yako kushawishi wengine katika kupunguza pengo kati ya biashara na umisheni.

Kehinde Ojo ni Mkurugenzi wa Programu ya Mpango wa Kusaidia Maendeleo ya Wenyeji. Michango yake ya awali kwa AfriGO ni pamoja na ‘Kupalilia Roho ya Ukarimu’ (sehemu ya 1 toleo la 4). Wasiliana naye kwenye: kehinde.ojo@ifeworld.org.

share
share
Instagram
contact us
contact us
contact us